Friday 23 June 2017

DAKIKA 120 ZA MWANDISHI WA JIBU NDANI YA HEKALU LA FREEMASON



 Jengo la Freemason liliopo Dar es Salaam, ambalo ndio la kwanza kabisa kutumiwa na Bunge la Tanganyika.


WATU wengi wanazungumzia kuhusu imani ya kundi la Freemason, huku baadhi wakihofu kuingia kwenye hekalu lao lililoko mjini Posta jijini Dar es Salaam, mwandishi wa Jibu la Maisha Denis Massawe, ameingia humo na hapa anaeleza alichokikuta. 
Kama kuna jambo la kijasiri nililowahi kufanya ambalo sitalisahau maishani ni pamoja na maamuzi ya kuingia ndani ya hekalu la Freemason lililoko mtaa wa Ohio mjini Posta jijini Dar es Salaam.
Nasema ni la kijasiri kwa sababu, nilipoanza safari yangu kutoka Ubungo kuelekea kwenye jengo hilo kichwani nilikuwa na maswali mengi yasiyo na majibu sahihi yaliyotokana na habari nyingi mbaya zinazoandikwa na picha za kutisha zinazohusu kundi hilo.
Lengo kubwa la safari yangu ilikuwa ni kujionea mwenyewe kwa macho yangu  shughuli zinazoendelea ndani ya jengo hilo, na kupata uhakika ili nisiwe mtu wa kusimuliwa tu.
Safari yangu ilafanyika siku moja baada ya kuzikwa kwa kiongozi wao mkuu mstaafu wa kundi hilo Andrew Chande aliyefariki dunia hivi karibuni.
 Pamoja na mambo mengine ya kitafiti niliyohitaji kujua pia nilitaka kufahamu  walipokeaje pole za Viongozi wa dini mbalimbali kufuatia kifo cha kiongozi wao Sir. Chande, ambae alifariki akiwa Nairobi nchini Kenya.
Licha ya kuwa na ujasiri mkubwa juu ya kutaka kuyafahamu hayo yote tena nikiwa kwenye eneo husika,  lakini pia nilijawa na hofu juu ya kile nilichohisi ‘kutolewa kafara’.
Nakumbuka siku moja kabla ya kufika katika jengo la ‘Freemason Hall’ nilipitia kwenye ofisi za Idara ya habari Maelezo mjini Posta, ambapo waandishi huwa na kawaida ya kukutana kwa lengo la kupeana vyanzo vya habari.
 Nilichohitaji kwao ni walau nijue kama kuna mwandishi aliyewahi kuingia katika jengo hilo.
Nilipofika Maelezo nilimkuta rafiki yangu ambae ni mwandishi wa gazeti la Jambo leo (jina namhifadhi), nikamuuliza hivi, ulishawahi kuingia kwenye jengo la Freemason Hall?’ Ghafla nilishangaa kuona jinsi alivyoshitushwa na swali hilo!   Akanijibu ‘wewe, unataka kwenda huko’ nilimjibu ndiyo.
 Akaniambia, wewe, ukienda huko ukirudi hapa ukiwa mzima basi nitajua kuwa ni mwanamume kweli. Akaendelea kunijuza, na ujue kuwa pale kuna njia ya chini kwa chini kutoka hotel ya Kilimanjaro maarufu Kempisk, hadi katika jengo hilo.
Rafiki yangu huyo alinikanya na kunipa angalizo akisema, angalia wasije kukupoteza. Kwakweli  kwa maneno ya rafiki huyo japo yalizidi kunitia hofu lakini hayakukata kiu yangu ya kwenda kutafiti niliyoyataka kwenye jengo hilo.
Baada ya kusikia nasaha hizo za rafiki huyo, ndipo nikaendelea na safari yangu lakini nilipofika katika ubalozi wa Zambia..Itaendelea kesho
Share:

0 comments:

Post a Comment

Ads

Blog Archive