Thursday 24 August 2017

HUYU HAPA BINGWA WA VPL MSIMU HUU



 
ACHANA na Ibrahim Ajibu au Haruna Niyonzima. Achana na Joseph Omog na George Lwandamina. Achana na TFF na Bodi ya Ligi, njoo uwanjani.
Pamoja na mbwembwe, maneno, kejeli, tambo na yote ya aina hiyo, mwisho wa msimu bingwa wa Ligi Kuu Bara anatakiwa kuwa mmoja tu. Ni nani ataondoka na taji hilo lenye heshima zaidi katika soka la Tanzania? Kazi ipo.
Tathmini inaonyesha kwamba vita kubwa ya ubingwa itakuwa kwa timu nne tu kati ya 16 zitakazoshiriki. Timu nyingine zinategemewa kukamia mechi moja moja na kujiepusha na janga la kushuka daraja.
Timu kama Lipuli, Ndanda, Majimaji na Stand United, zinatazamiwa kuendelea kuwa wasindikizaji na kutumia muda mwingi katika eneo la chini badala ya kuwania ubingwa.
Timu za Mtibwa Sugar, Mbeya City na Mwadui zinatarajiwa kuwa katika eneo la katikati muda mwingi wa msimu huu, kutokana na kuwa na uwekezaji wa kawaida ambao hautoshi kuwasaidia kushinda ubingwa.
Timu zinazowania ubingwa sasa ni zipi? Mwanaspoti inakuletea tathmini wakati huu ambapo pazia la Ligi Kuu linakwenda kufunguliwa kesho Jumamosi.
Simba 9/10
Tathmini mpaka sasa inaonyesha kwamba Simba ndiyo timu yenye nafasi kubwa zaidi ya kushinda taji la Ligi Kuu kwa msimu huu mpya.
Simba imesajili wachezaji 13 ambao ni makipa; Aishi Manula kutoka Azam, Said Mohammed ‘Nduda’ kutoka Mtibwa na Emmanuel Mseja kutoka Mbao FC. Timu hiyo imesajili pia mabeki; Yusuf Mlipili kutoka Toto Africans, Ally Shomary na Salim Mbonde kutoka Mtibwa.
Nyota wengine waliotua Msimbazi ni mabeki; Shomary Kapombe na Erasto Nyoni kutoka Azam na Jamal Mwambeleko kutoka Mbao FC. Pia kuna kiungo Haruna Niyonzima kutoka Yanga. Wengine ni washambuliaji John Bocco kutoka Azam, Emmanuel Okwi kutoka SC Villa ya Uganda na Nicholas Gyan kutoka Ghana.
Usajili wa Simba unaonekana kuwa na nguvu hasa katika nafasi ya ulinzi ambayo sasa itakuwa chini ya watu 12 wa nguvu, ambapo mabeki ni tisa na makipa ni watatu.
Eneo la kiungo nalo limeimarishwa kwa kuongezwa Niyonzima ambaye ametamba na Yanga kwa miaka sita na kushinda mataji tisa ya Ligi Kuu. Eneo hilo tayari lilikuwa na wakali kama Jonas Mkude, Mzamiru Yassin na James Kotei.
Kwa namna ya upana wa kikosi cha Simba, ni wazi kwamba inaweza kupambana wakati wote wa Ligi na kushinda taji hilo.
Kitu kingine ambacho kinaipa nguvu ni uwezo mkubwa kifedha ambao inao kwa sasa ambapo mbali na kupata fedha za udhamini kutoka SportPesa, Vodacom na Azam TV, pia wanafadhiliwa na bilionea Mohammed Dewji.
Yanga 8.5/10
Mabingwa mara tatu mfululizo wa Ligi Kuu Bara, Yanga, nao wana nafasi kubwa ya kutetea tena taji lao. Yanga bado ina kikosi imara cha kuweza kuwania taji hilo lakini italazimika kupambana na Simba imara.
Katika usajili wake, Yanga, imeimarisha maeneo yenye uhitaji maalumu kwenye kikosi chake ambapo imemsajili beki wa kati, Abdallah Shaibu ‘Ninja’ kutoka Zanzibar ili kuwaongezea nguvu Nadir Haroub ‘Cannavaro’ na Kelvin Yondani.
Timu hiyo imesajili pia viungo wawili wa shoka ambao ni Raphael Daudi kutoka Mbeya City na Kabamba Tshishimbi ‘Papii’ kutoka Mbabane Swallows ya Swaziland huku pia ikiwaongeza Baruan Yahya na Ibrahim Ajibu kwenye safu yao ya ushambuliaji.
Pigo kubwa kwa Yanga ni kuondoka kwa winga wake tegemeo, Simon Msuva aliyejiunga na El Jadida ya Morocco. Msuva ameifungia Yanga mbaao 40 Ligi Kuu katika miaka mitatu iliyopita jambo ambalo linatosha kuonyesha umuhimu wake.
Nguvu kubwa ya Yanga itaendelea kuwa katika safu ya ushambuliaji chini ya kinara Amissi Tambwe ambaye atafanya kazi kwa ukaribu na Donald Ngoma na Obrey Chirwa.
Singida United 8/10
Timu hii inarejea Ligi Kuu baada ya muda mrefu, lakini tathmini inaonyesha kwamba ina nafasi pia ya kutwaa taji hilo. Baada ya Simba na Yanga, timu inayopewa nafasi kubwa ya kuondoka na taji hilo ni Singida United.
Timu hiyo imefanya usajili wa nyota zaidi ya 14 jambo linaloifanya kuwa na ushindani mkubwa. Miongoni mwa nyota makini ambao wamejiunga nao ni, Elisha Muroiwa na Muzdafa Kotinyu kutoka Zimbabwe pamoja na Danny Usengimana na Michael Rushegoga kutoka Rwanda.
Singida imesajili kikosi kipana na bila shaka kocha, Hans Van Pluijm, atakuwa na chaguo la kutosha katika kila eneo, tofauti na timu nyingine za Ligi Kuu.
Silaha kubwa ya Singida inatarajiwa kuwa soka la kushambulia kwa kasi hasa kupitia pembeni, soka maarufu la Pluijm ambaye aliipa Yanga mataji mawili mfululizo kabla ya kuhamia Singida.
Azam 8/10
Matarajio makubwa yaliyokuwapo kwa Azam FC sasa yameondoka hasa baada ya timu hiyo kuondokewa na mastaa wake sita wa kikosi cha kwanza ambapo wanne kati yao wamejiunga na Simba.
Nyota walioondoka ni kipa Aishi Manula, mabeki Erasto Nyoni na Shomary Kapombe pamoja na mshambuliaji John Bocco waliotua Simba. Hata hivyo bado Azam inaonekana kuwa na kikosi cha ushindani ambacho kinaweza kuwashangaza wengi na kuondoka na taji hilo.
Usajili wa Azam si wa mbwembwe tofauti na ilivyokuwa katika misimu michache iliyopita. Msimu huu imemsajili kipa Benedict Haule kutoka Mbao FC, Hamimu Abdulkarim kutoka Toto Africans, kiungo Salimin Hoza kutoka Mbao FC pamoja na washambuliaji Waziri Junior kutoka Toto na Mbaraka Yusuf kutoka Kagera Sugar.
Bado Azam inaendelea kuwa na timu imara, lakini nafasi yake ya ubingwa haiwezi kuwa kubwa hasa kutokana na wapinzani wake wa karibu, Simba na Yanga kujipanga vyema. Njia pekee ya Azam kutwaa taji ni pale wapinzani wake  watakapofanya vibaya.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Ads

Blog Archive