Friday 1 September 2017

SIMBA YAZIDI KUIACHA YANGA MATAA


WAKATI Yanga ikiwa katika usingizi wa pono, watani zao Simba wapo mbioni kutengeneza mamilioni ya fedha kupitia mtaji wa mashabiki wao ndani na nje ya nchi.
Simba iliyopo katika hatua nzuri ya kuhama kutoka mfumo wa wanachama kwenda katika Hisa, inatarajia kuingiza fedha za maana kutokana na uwekezaji wake katika digitali.
Mpaka sasa, Simba inayoongoza kwa mapato ya nje ya uwanja ikiwa inaingiza Sh351 milioni kutoka katika majengo yake pale Kariakoo, Sh100 milioni ya kipindi cha Simba TV kinachorushwa moja kwa moja na Azam TV.
Simba inayoongoza kwa kutwaa mataji ya Afrika Mashariki na Kati (Kagame Cup) ikifanya hivyo mara sita, inaingiza pia zaidi ya Sh36 milioni kwa mauzo ya jezi zake, pia ikipanga kuboresha zaidi biashara hiyo ili ivune maradufu tofauti na sasa.
Ukiachana na fedha hizo za mboga hapo juu, Simba iliingia mkataba wa biashara na kampuni ya EAG Group ambayo sasa iko mbioni kufanya biashara ya digitali ambayo itaipa klabuni hiyo mamilioni na kuifanya kuwa kwenye anga za kimataifa.
Uwekezaji Simba App
Simba inatarajiwa kupiga mkwanja wa maana kupitia Simba APP ambayo inatoa taarifa rasmi za klabu hiyo kwa gharama nafuu ukilinganisha na vyanzo vingine vya habari.
App hiyo ambayo ipo chini ya EAG Group tayari imepakuliwa na watu 121,000, ikiwa ni miezi mitano tu tangu kuzinduliwa.
Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Imani Kajula anasema kwa siku kati ya watu 1,000-2,000 wanapakua App hiyo jambo ambalo linawapa imani kwamba huenda wakafikia watu 200,000 mwakani.
“Sio uwekezaji mdogo, mpaka sasa tumetumia zaidi ya Sh 400 milioni kuifikisha App hapo ilipo. Imefanyiwa kazi na watu kutoka Afrika Kusini na Israel, inahitaji uvumilivu na subiri kufanya hii biashara,” anasema Kajula.
“Tunatazamia idadi ya watu itaongezeka zaidi. Kwa sasa tunapatikana kwenye simu za Android, lakini tumeanza pia mchakato wa kuitengeneza App itakayotumika pia kwenye simu za Apple na nyingine za Kimarekani,” anaeleza.
Kuonyesha mechi
Kajula anasema tayari kampuni yake imeingia makubaliano na Azam TV, ili kuweza kuonyesha mechi za Simba za Ligi Kuu Bara pamoja na zile za hatua za awali za mashindano ya kimataifa na kwa kila mechi mtu atalipia Sh1,000.
“Tayari tumenunua vifaa vya kurusha mechi moja kwa moja na kwa wiki sasa tumekuwa tukivifanyia majaribio. Vilichelewa kidogo, tulipanga kuanza navyo wakati wa Simba Day,” anaeleza.
“Tunatazamia kama robo ya watu waliopakua App yetu watatazama mechi basi tutakuwa tunaingiza hadi Sh40 milioni kwa mechi moja,” anasema.
Kutokana na makadirio hayo, huenda App hiyo ikaingiza hadi kiasi cha Sh600 milioni kwa mwaka kutokana na kazi hiyo ya kuonyesha mechi, endapo robo tu ya watu waliopakua App hiyo watalipia kuona mechi.
Malipo ya Kawaida
Mbali na kuonyesha mechi, Simba APP kwa sasa inatoa taarifa rasmi za Simba, picha za mnato na video za mahojiano na wachezaji pamoja na watu wa Simba, habari ambazo kwa mwezi zitakuwa zikilipiwa Sh2,000 tu.
“Kama nusu tu ya watu waliopakua App watalipia, basi tutapata zaidi ya Sh120 milioni kwa mwezi,” anasema.
Kwa sasa App ya Simba ina kurasa nne ambazo ni Simba News inayotoa taarifa za maandishi na picha za mnato, Simba Live inayotoa matukio ya video ya timu hiyo ambapo, wameunganisha na mtandao wa Youtube.
Ukurasa mwingine ni Simba Exclusive na huwekwa video za mahojiano maalumu na wachezaji na viongozi wa klabu hiyo. Kwa makadirio huenda App hiyo ikawa inaipatia Simba zaidi ya fedha za udhamini wa SportPesa sasa ambao kwa mwaka wamewapa Sh950 milioni.
Simba Day
Kampuni hiyo ya EAG ndiyo imekuwa ikisimamia tamasha la Simba Day ambapo, mwaka huu limeweka rekodi ya kupata watazamaji 52,000, idadi kubwa kuliko wanaojitokeza kutazama mechi za Simba na Yanga sasa.
“Ukitazama kwa nje unaweza kuona kawaida, lakini tumeweka fedha nyingi katika matangazo na kuitangaza Simba Day. Mwaka jana tulikuwa na watazamaji 46,000 lakini namba imeongezeka sana mwaka huu.
“Gharama zilikuwa ni nyingi, tumetangaza kwenye redio na televisheni, tuliwatumia pia mastaa kadhaa. Pia kuwaleta Rayon Sports hapa ilikuwa gharama kubwa,” anaeleza.
Mauzo ya jezi
“Tunashukuru Simba imeanza kupata faida kutokana na jezi zake. Changamoto ni nyingi na bado hatujaweza kufikia juu sana, lakini tunakwenda vizuri. Mfano sasa jezi ya Simba inavutia, inapendwa sana na mashabiki.
“Tunazidi kuimarisha maeneo kadhaa, lakini hata hivyo natazama zaidi hili soko la kwenye mtandao, App itatupa fedha nyingi. Tunataka kuuza tiketi za mechi za Simba kwenye App yetu pia, tunatengeneza viza kwa watu wa nje waweze kulipia,” anaeleza.
SOURCE; MWANASPOT
Share:

0 comments:

Post a Comment

Ads

Blog Archive