Friday 15 September 2017

MAYWEATHER AFUNGUKA HAYA KUHUSU MAISHA, NGUMI NA ELIMU YAKE

Bondia Floyd Mayweather.

BONDIA Floyd Mayweather amefunguka mengi kuhusu maisha yake ya ndondi na binafsi ikiwemo kuhusu kama atarejea kwenye ndondi au ndiyo amestaafu ukweli.
Mayweather ambaye alitangaza kustaafu kupigana mwaka 2016 kisha kuamua kurejea mwaka huu na kupigana pambano dhidi ya Conor McGregor likiwa ni pambano lake 50, inaaminika ndiye bondia mwenye mafanikio makubwa kifedha kuliko wote kuwahi kutokea.
Katika pambano hilo lililopewa jina la pambano la fedha, Mayweather alishinda na hivyo kujiandikia rekodi ya kucheza mapambano 50 akishinda yote, huku akiingiza kiasi kikubwa cha fedha kutokana na mikataba mbalimbali.
Akifanya mahojiano na mtangazaji Diego wa kwenye mtandao wa YouTube ambaye amekuwa ni maarufu kwa kutumia kuhoji kupitia katuni (yaani katuni ndiyo inakuwa kama inazungumza na mgeni), Mayweather amedai kuwa hadi sasa ana wapenzi saba na ana magari 25 ya kifahari ambayo yote yapo Las Vegas.


Magari hayo ni yale ambayo anayo kwenye jiji hilo tu, yakiwemo Bugatti na Ferrari ambayo thamani yake ni zaidi ya shilingi bilioni 1 kila moja.
Mayweather amesisitiza kuwa, pambano lake na McGregor lililofanyika mwezi uliopita ndilo lilikuwa la mwisho kwake na hana mpango wa kurejea ulingoni kupigana.
“Hilo lilikuwa pambano la mwisho kwangu kupigana, uhakika hilo lilikuwa la mwisho, pambano lijalo labda nitapigana katika dunia nyingine,” anasema Mayweather ambaye elimu yake ya dunia ni ya kawaida kwa kuwa aliacha shule mapema na kujiingiza kwenye ndondi.
Mahojiano hayo yalifanyika mbele ya ukumbi wa usiku wa Mayweather unaojulikana kwa jina la Girl Collection unaopatikana Las Vegas.


Alipoulizwa kuhusu mpenzi wake, alisema yeye ni mwanaume ambaye hawezi kuwa mwaminifu kwa mwanamke mmoja.
“Nina wanawake wangapi? Nafikiri ni kama saba hivi ambao wana bahati kuwa na mimi.
“Huwa nikiamua ninatoka na mmoja wao kwenda kula, mwingine tunasafiri pamoja, kuwa na mwanamke mmoja ni sawa na kutokuwa na mpenzi kwa kuwa muda wowote unaweza kumkosa,” anasema.
Alipoulizwa juu ya kiasi cha fedha ambacho anacho kwenye akaunti zake, Mayweather alisema anazo akaunti kadhaa za benki na hakumbuki hasa salio lake katika kila akaunti.


“Nina zaidi ya dola milioni 200 nyingine dola milioni 300,” anasema bondia huyo ambaye licha ya kujulikana kupenda kuonyeshea fedha zake lakini pia ni hodari katika kupambana kutafuta mafanikio hasa kwenye suala la ndondi.
Ikumbukwe kuwa katika pambano lake la mwisho dhidi ya McGregor, bondia huyo Mmarekani inaelezwa kuwa aliingiza zaidi ya pauni milioni 100 ndani ya usiku mmoja tu.
Alipoulizwa juu ya ushauri anaoweza kutoa kwa mwanaume aliyeoa, akashauri huku akicheka kwa kusema: “Mpe talaka mkeo.”
“Ukitaka kumwambia au kutafuta njia ya kumuacha mkeo, mlete kwenye hii klabu yangu (ni klabu ya wanawake wanaocheza wakiwa nusu utupu) kisha mwambie ni sehemu pekee ambayo huwa unapenda kuitembelea. Ukifanya hivyo hutakuwa na haja ya kumpa talaka, ataondoka mwenyewe.”
Kutokana na kauli yake ya kuwa na uhusiano na wanawake saba, tujikumbushe baadhi ya wanawake maarufu aliowahi kuwa na uhusiano nao na baadhi bado yupo kwenye uhusiano nao wa kimapenzi:
Abi Clarke
Huyu ni mtangazaji wa runinga na staa wa showbiz ambaye inaelezwa kuwa amekuwa na uhusiano na Mayweather, hawajawahi kuweka wazi lakini taarifa zimekuwa zikijulikana wawili hao wana uhusiano. Uhusiano wao ulianza mwaka jana wakati Abi alipokuwa Las Vegas kwa ajili ya mapumziko.


Rmarni Ellis
Binti huyu ni raia wa Uingereza ambaye ana umri wa miaka 20, alikutana na Mayweather wakati bondia huyo alipotembelea nchini mwake. Inadaiwa uhusiano wao uliisha kimyakimya lakini hakuna taarifa zaidi.
Mara baada ya kukutana Uingereza, Mayweather akamsafirisha Rmarni hadi Marekani ili waweze kuwa pamoja.
Licha ya ubilionea wake alionao lakini Mayweather alianguka kwenye penzi la mrembo huyu ambaye kazi yake ni kuuza dukani na ambaye alikuwa akilipwa pauni 6.50 kwa saa.
Binti huyo ambaye naye ana umri wa miaka 20 alikutana na bondia huyo kwenye mishe zake hizohizo za dukani.
Yahaira Vianne Ochoa
Huyu ni mwanamitindo ambaye hata baada ya pambano lake la mwisho, wawili hao walionekana kuwa pamoja na walipiga picha wakiwa pamoja
Doralie Medina
Huyu amedumu muda mrefu kidogo na Mayweather na mara kadhaa aliwahi kuonekana hadharani akiwa na bondia huyo.
Medina anajulikana kwa kuwa na umaarufu mkubwa kwenye mitandao ya kijamii. Inaelezwa kuwa mrembo huyu anajua vizuri kuzitumia fedha za Mayweather. Mwaka 2014 katika tuzo za BET, mrembo huo aliingia ukumbini akiwa ametupia nguo za dola 70,000.
Alikuwa ametupia vitu vingi vya thamani kubwa ikiwemo cheni na viatu. Pia Mayweather aliwahi kumnunulia gari aina ya Rolls Royce wakati wa siku yake ya kuzaliwa Julai 2014.
Melissa Brim
Huyu ni mama wa mtoto wake wa kike, waliachana na kama ilivyo kawaida ya mastaa wengi, amekuwa na migogoro ya mara kwa mara na mzazi mwenza huyu.
Josie Harris
Huyu pia ni mzazi mwenza wa bondia huyo, hawapo pamoja lakini mara kadhaa aliwahi kutofautiana na Melissa Brim, walishambuliana mitandaoni kisa kikiwa ni wivu wao kwa Mayweather.
Alidumu na Mayweather kwa miaka mingi tangu akiwa anachipukia kwenye ndondi lakini anakiri kuwa uhusiano wao ulivurugika na wakatofautina kwa kuwa maisha yake hayakuwa mazuri pindi akiwa ndani ya penzi la bondia huyo.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Ads

Blog Archive