Friday 29 September 2017

KATIBU ABAINISHA KINACHOISULUBU YANGA SASA

Lwandamina na Nsajigwa wakimfunda Mwashiuya
Lwandamina na Nsajigwa wakimfunda Mwashiuya wakati tizi likiendelea kwenye manyunyu jijini Dar es Salaam. 
KATIBU wa zamani wa Yanga, Abdul Sauko, ametamka wazi kwamba kinachotokea kwenye klabu hiyo kwa sasa, ni matokeo ya kukosa watu wenye mapenzi ya dhati ya kujitolea kwa moyo kama tofauti na zamani na ndio maana timu inayumba nje ya uwanja.
Sauko aliyeshikilia nafasi mbalimbali za ukatibu klabu hapo miaka ya nyuma, alisema katika uongozi wao waliwatafuta matajiri na kuwajengea moyo wa kujitolea, jambo lililoisaidia Yanga kiasi cha kutisha Afrika Mashariki na Kati mpaka kupachikwa jina la Yanga Afrika Umoja wa Mataifa.
Alisema bado kuna watu ambao  wanaweza kutoa michango yao kwa timu, lakini akadai baadhi ya viongozi hawajajiweka karibu na watu hao ili kuonyesha umuhimu wao ndani ya timu na kusaidia kujitoa kwa hali na mali.
“Sisi tuliwatafuta na kuwaweka karibu, ndiyo maana wakati ule hata pesa za usajili tulichangishana kuhakikisha timu inafanya vizuri,” alisema Sauko ambaye alikuwa miongoni mwa waasisi wa kundi la Yanga Family ambalo lilikuwa mhimili wa usajili mwanzoni mwa miaka ya 2000.
“Wachezaji na wafanyakazi kwa ujumla wakitimiziwa mahitaji yao, watajituma kikamilifu.
“Mipango ya timu ilikuwa wazi kwao, ndicho kilichokuwa kinawafanya wawe na uchungu wa kuona inapotokea timu ikatetereka kwa masuala ya fedha, inakuwa aibu kwao, hilo linapaswa kufanywa kwa sasa. Hata nafasi za ujumbe ndani ya klabu zilishikwa na watu ambao walikuwa tayari kujitolea kutatua shida ndogo ndogo. Hilo pia lilikuwa msaada kwa timu kiasi cha kuwa na mafanikio ya hali ya juu.”
Sauko aliwataka viongozi waliopo madarakani Yanga kwa sasa, wawasake wadhamini ambao watabeba gharama za klabu kwa asilimia 80, watafanya wachezaji wapate mishahara kwa wakati, wasafiri kwenda mikoani, huku asilimia 20 ya gharama, ziwe za wanachama kujitolea, uuzwaji wa jezi pamoja na pesa za viingilio vya timu inapofanya mazoezi.
“Ni kutengeza mipango madhubuti, wanachama wanapenda timu zao, wapo tayari kutoa viingilio vya mazoezi, hivyo wanaweza kupata pesa ndogo ndogo za kukidhi mahitaji yao, naamini hilo litawapa hatua.
“Tulikuwa tunatangaza viingilio pindi timu ikifanya  mazoezi Uwanja wa Kaunda, mashabiki walikuwa wanakuja, tena wengine kutoka mbali, hasa kipindi cha usajili ndipo tulipata pesa zaidi kutokana na mashabiki kuwa na hamu ya kuwaona wachezaji wapya.
“Lazima unapopanga bajeti ya mwezi kwa klabu kama Yanga, uwe na miradi ama vyanzo vya kupata pesa,  lasivyo mipango itakuwa inaingia doa na kushindwa kufikia pale panapotakiwa.
“Najua maneno haya hayatawafurahisha wengi lakini ndiyo ukweli.”
Share:

0 comments:

Post a Comment

Ads

Blog Archive