Monday 14 August 2017

SAMATTA, MSUVA, FARID WAFUNIKA ULAYA

Wachezaji wa Kitanzania wanaocheza mpira wa kulipwa nje ya nchi ameanza kutikisa barani Ulaya mwishoni mwa wiki katika michezo ya ligi pamoja na mechi za kirafiki za kujiandaa na msimu mpya wa ligi mbalimbali. 
Ubelgiji
Nahodha wa Taifa Stars, Mbwana  Samatta ameanza kufungua kapu lake la mabao baada ya kufunga goli mbili na kuiongoza Genk kushinda 5-3 dhidi ya Royal Antwerp FC katika mchezo wa Ligi Kuu ya Ubelgiji ‘Jupiler Pro’.
Katika mchezo huo Samatta alifunga mabao yake katika dakika 8 na 41 na kuifanya Genk kupata ushindi wake wa kwanza tangu kuanza kwa ligi hiyo ikiwa imecheza mechi tatu ikifungwa moja kutoka sare moja na kushindi moja.
Hispania
Mshambuliaji Simon Msuva ni kama amejibu mapigo ya Samatta kwa kufunga juzi nchini Hispania katika mchezo wa kirafiki.
Msuva yupo Hispania na timu yake ya Difaa Hassani El Jadidi akijiandaa na Ligi Kuu Morocco ‘Batola Pro’.
Msuva  amedai licha ya kupoteza mchezo huo kwa mabao 2-1 na  USMO,  timu yake ilicheza vizuri  lakini haikuwa na bahati ya kushinda mchezo huo.
“Ni vikosi viwili vilitumika kama ilivyokuwa kawaida yetu, kila kikosi kilipata dakika 45, nimefunga bao ambalo halikutosha kutufanya tusipoteze” alisema Msuva.
Naye Mtanzania Farid Mussa anayecheza CD Tenerife alishindwa kuisaidia timu yake isiepuke kipigo cha mabao 3-0 kutoka kwa Deportivo La Coruna katika mchezo wa kirafiki.
Kiwango alichoonyesha Farid katika michezo ya kirafiki msimu huu kinafungua milango kwake kucheza kikosi cha kwanza cha Tenerife katika ligi ya Segunda watafungua dhidi ya Real Zaragoza, Agosti 18.
Ureno
Mtanzania  Orgenes Mollel ilicheza timu yake Famalicao ikilazimishwa sare 1-1 na Penafiel katika mchezo wa Ligi daraja la pili nchini Ureno ‘Segunda Liga’ya uliofanyika Agosti 13 ugenini kwenye Uwanja wa Municipal.
Mollel mwenye miaka 19 amekuwa na changamoto ya kuanza katika kikosi cha kwanza cha timu hiyo ambayo inashika nafasi ya tatu ikiwa na pointi nne (4) katika msimamo wa Ligi hiyo.
Ujerumani
Beki wa kushoto Emily Mgeta aliingoza VfB Eppingen kupata ushindi mnono wa mabao 4-1 dhidi ya Oeffingen katika mchezo wa kirafiki nchini Ujerumani.
“Huo ndiyo mchezo wetu wa mwisho maana wiki ijayo tunaanza ligi, kikubwa tulichopanga ni kupanda daraja, tumefanya maandalazi ya kutosha na hata  tulivyoweka kambi  nchini Italia kulikuwa na sababu.” alisema beki huyo wa zamani wa Simba.
Austria
Kinda la Kitanzania, Michael  Lema anayeichezea  SK Sturm Graz ya Austria amepata majeraha ya kifundo cha mguu yatayomweka nje kwa wiki mbili au zaidi.
Lema alisema hajui ni lini atarejea uwanjani, lakini amekuwa akitajwa kuwa huenda akaanza mazoezi mepesi ndani ya wiki tatu zijazo.
“Niliumia mazoezini naendelea vizuri maana mwanzo ilidhaniwa kuwa ni majeraha makubwa, lakini imekuwa tofauti,” alisema Lema.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Ads

Blog Archive