Tuesday 29 August 2017

LISSU ARIPOTI POLISI NA KUAMBIWA......


Mwanasheria Mkuu wa Chadema, Tundu Lissu ameripoti jana Kituo Kikuu cha Polisi na ametakiwa kuripoti tena Septemba 11.


Kaimu Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Benedict Kitalika amesema mwanasiasa huyo alifika kituoni jana Agosti 28 mchana kama alivyotakiwa na jeshi hilo.

"Nimeongea na msaidizi wa ZCO (Mkuu wa Upelelezi Kanda) anasema ameripoti . Muda umesogezwa sana kwa sababu kuna majukumu mengine yanashughulikiwa kwa sasa," amesema Kitalika.

Lissu ambaye pia ni Mbunge wa Singida Mashariki, alikamatwa na polisi mwishoni mwa wiki iliyopita akiwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akituhumiwa kumkashifu Rais John Magufuli wakati wa mkutano wake na waandishi wa habari kwenye hoteli ya Protea siku chache zilizopita.

Siku ya mkutano huo, Lissu aliibua sakata linalohusu kampuni ya Stirling Civil Engineering Ltd (SCEL) kushikilia ndege ya Bombardier Dash 8 nchini Canada hadi Serikali itakapoilipa deni la Sh87 bilioni. 

Katika sakata hilo, Lissu alimhusisha Rais ambaye wakati huo alikuwa waziri wa ujenzi kwa kuvunja mkataba wa ujenzi wa Barabara ya Tegeta Wazo Hill -Bagamoyo iliyokuwa ikijengwa na SCEL.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Ads

Blog Archive