Tuesday 25 July 2017

OMOG AWANYIMA RAHA YANGA


Kiungo Mnyarwanda, Haruna Niyonzima.
TAARIFA za ujio wa kiungo Mnyarwanda, Haruna Niyonzima ndani ya Simba zimemkosha kocha wa timu hiyo, Joseph Omog raia wa Cameroon ambapo ameweka wazi ya moyoni kuwa nyota huyo atawasaidia msimu ujao.

Niyonzima anadaiwa kumalizana na viongozi wa Simba kwa ajili ya kukichezea kikosi hicho kilichopo nchini Afrika Kusini katika msimu ujao wa 2017/18 akitokea kwa wapinzani wao, Yanga.

Kocha huyo aliyeipa ubingwa wa FA Simba msimu uliopita, ameliambia Championi Jumatatu kuwa, kama kweli kiungo huyo anajiunga nao basi Simba itatisha na itawatambia wapinzani wao kwa msimu ujao kutokana na uwezo wake mkubwa hasa katika kutengeneza nafasi za kufunga.

“Ikiwa kweli Niyonzima anatua kwetu basi nakwambia tutatisha sana msimu ujao na wapinzani wetu wajiandae kuumia kwani kiungo huyo ni moja ya wachezaji wenye vipaji vya hali ya juu na hakuna kocha ambaye atakataa kuwa naye kwenye kikosi chake.
“Kila mmoja anajua uwezo wake mkubwa wa kupiga pasi zenye macho na anapoongezeka ina maana kwamba washambuliaji wetu watakuwa wanapata pasi nyingi za kufunga na kusababisha tuwe tunashinda katika michezo yetu mingi.


“Kikubwa nasubiri kuona kama atatua maana mpaka sasa sijajua kama ni kweli au la, lakini pia naendelea kukinoa kikosi changu kuhakikisha kinakuwa na makali na kufanya vizuri kwenye mechi zake ikiwemo ya Simba Day,” alisema Mcameroon huyo.

Katika maelezo yake, Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hans Poppe, juzi alisema wameshazungumza na mchezaji huyo lakini hakufafanua zaidi huku akisema kuna wachezaji wawili wanawataka na bado wana mikataba na timu zao za zamani, hivyo hawawezi kuwataja kwa sasa.

Ikumbukwe kuwa pia, Simba inatajwa kumalizana na Aishi Manula ambaye pia bado ana mkataba na Azam FC lakini ameshaweka wazi kuwa ataondoka klabuni hapo na inavyoonekana kuwa atatua Msimbazi pamoja na Niyonzima.
Share:

1 comment:

Ads

Blog Archive