Saturday 30 September 2017

HIZI NDIYO WIKI ATAKAZOKAA NJE AGUERO

MSHAMBULIAJI Sergio Aguero anahitaji angalau wiki nne za mapumziko baada ya kuvunjika mbavu katika ajali ya gari usiku wa juzi mjini Amsterdam.
Mchezaji huyo wa Manchester City aliumia Alhamisi wakati teksi aliyokuwa amepanda yeye na rafiki yake kwenda Uwanja wa Ndege ilipoacha barabara na kugonga nguzo pembeni.

Muargentina huyo ambaye alikuwa katika siku yake mapumziko, alikwenda kushuhudia tamasha ingawa ilikuwa ndani ya saa 48 kabla ya City hauijavaana na Chelsea leo jioni katika mchezo wa Ligi Kuu ya England Uwanja wa Stamford Bridge.

Kocha wa City, Pep Guardiola alisema jana kwamba hana tatizo na mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 29 kusafiri katika siku yake ya mapumziko ingawa pia alisema hakuwa na taarifa za safari ya Aguero.

Usiku wa Ijumaa, Aguero alitweet picha yake akionyesha dole gumba juu sambamba na maelezo: "Nipo nyumbani Manchester baada ya kufanyiwa vipimo na madaktari wa klabu. Nimevunjika mbavu. Nimeumia, lakini niko salama, naangalia namna ninavyopata nafuu. Asante kwa wote walionitumia ujumbe na kunisapoti,"alisema.

Baada ya kuangalia tamasha la mwanamuziki wa Colombia, Maluma, Aguero na rafiki yake walikuwa wanakwenda Uwanja wa Ndege Saa 7:00 usiku kuchukua ndege binafsi kurejea Manchester wakati teksi inaacha barabara na kugonga nguzo.

Akifafanua kilichotokea, Aguero alitweet: "Teksi niliyopanda ilikosea kugeuka ikagonga nguzo. Ulikuwa ni mshindo mkubwa, lakini mkanda wa kiti ulinisaidia kutoumia zaidi,".

Alipoulizwa kuhusu safari ya Aguero Uholanzi, Guardiola alisema: "Mimi si Polisi. Nilijua nilipoamka. Sitaki kujua wachezaji wangu wanafanya nini,".
Share:

0 comments:

Post a Comment

Ads

Blog Archive