Tuesday 8 August 2017

MATOKEO BAADA YA MSHINDI WA URAIS KUTANGAZWA KENYA



Matokeo ya uchaguzi wa urais nchini Kenya yanaendelea kutangazwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (IEBC).
Mgombea wa urais anahitaji kushinda asilimia 50 na kura moja ili kutangazwa kuwa mshindi, na pia apate asilimia 25 katika angalau majimbo 24.
Ikiwa hakuna mgombea atakayepata kura nyingi, basi uchaguzi mpya kati ya wagombea wawili wanaoongoza utafanyika kabla ya siku 30 kutoka kura ya kwanza kupigwa kutimia.
Wachanganuzi wameigawana Kenya katika mikoa kanda tano kikabila: Kikuyu na makundi yanayohusiana nao (asilimia 21), Luhya (asilimia 14), Kalenjin (asilimia 13), Kamba (asilimia 10) na Luo (asilimia 10).
Uhuru Kenyatta na naibu wake wanarai jamii zao za Wakikuyu na Wakalenjin, wakati Raila Odinga na naibu wake, Kalonzo Musyoka (kutoka jamii ya Wakamba), wanatarajia kuungwa mkono na jamii za Waluo na Kamba.
Odinga pia anatarajia kupata kura nyingi kutoka jamii ya Waluhya. Musalia Mudavadi, ambaye aliwania urais mwaka wa 2013, na anatoka jamii ya Waluhya ni muhimu kwenye kampeni ya Raila Odinga.
Kura kadhaa za maoni zilionyesha ushindani mkali kati ya Kenyatta na Odinga, na kusababisha watu kuanza kufikiria matukio kadhaa yanayoweza kufuata baada ya matokeo ya kura kutangazwa.
1. Ikiwa hakuna mgombea kati ya wale wawili wanaoongoza atapata zaidi ya asilimia 50 ya kura. Uchaguzi mpya utaandaliwa kabla ya siku 30 kutimia.
A) Kenyatta anashinda uchaguzi wa marudio
B) Odinga anashinda uchaguzi wa marudio
2. Kenyatta anaibuka mshindi kwenye duru ya kwanza.
A) Odinga anakataa kukubali na kukata rufaa kwenye Mahakama Kuu.
B) Odinga anakataa kushindwa, anakataa kukata rufaa, na kuitisha maandamano, ambayo yanaweza kuzua vurugu.
3) Odinga anaibuka mshindi kwenye duru ya kwanza.
A) Kenyatta anakubali kushindwa.
B) Kenyatta anakataa kushindwa na kukata rufaa kwenye Mahakama Kuu.
Ikiwa Mahakama Kuu itatupilia mbali matokeo ya uchaguzi wa rais, kura zitapigwa upya kabla siku sitini kumalizika.
Atakayeibuka mshindi ataapishwa Jumanne ya kwanza, siku 14 baada ya matokeo ya uchaguzi kutangazwa.
……………………
Mfumo wa uchaguzi Kenya
Katiba ya 2010 ilianzisha serikali za majimbo nchini humo.
Kuna wapiga kura 19,687,563 waliosajiliwa ambao watachagua rais, magavana 47 wa majimbo, maseneta 47, wawakilishi wa wanawake 47, wabunge 290 na wawakilishi wa Bunge 1,450 .
Kuna wagombea 16,259 wanaoshindania nafasi hizi. Idadi kubwa kati yao ni wagombea wa kujitegemea.
IEBC imechapisha karatasi 20,818,000 za kura ya urais.
Upigaji kura umefanyika katika vituo 40,883 vya kupigia kura - kutoka vituo 24,563 vilivyotumika mwaka 2013.
IEBC ina wafanyakazi 360,000 wanaosimamia mchakato huu katika vituo vya kupigia kura.
Kura zilizopigwa zinahesabiwa kwenye vituo vya kupigia kura, na kupelekwa kwenye vituo vya majimbo, ambako zinajumlishwa na kutangazwa na afisa wa IEBC.
Matokeo yanayotangazwa katika eneo bunge yatakuwa ya mwisho, na yanapeperushwa hadi kwenye kituo cha kitaifa cha IEBC huko Nairobi
Kituo cha kitaifa cha IEBC katika Ukumbi wa Bomas ndicho kitakachotangaza matokeo ya mwisho ya kura ya rais.
Uchaguzi ulianza saa kumi na mbili asubuhi na vituo vingi vikafungwa saa kumi na moja jioni. Matokeo yalianza kupokelewa muda mfupi baadaye.
Sheria inaruhusu tume hiyo kutangaza matokeo kamili katika kipindi cha siku saba baada ya upigaji kura kumalizika.
IEBC imekuwa ikitumia mfumo wa dijitali unaoitwa Mfumo wa Usimamizi wa Uchaguzi wa Kenya (KIEMS) kuwatambua wapiga kura na kusambaza matokeo.
Umoja wa Mataifa, Umoja wa Ulaya na Umoja wa Afrika umetuma watazamaji kufuatilia uchaguzi.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Ads

Blog Archive