Tuesday, 1 November 2016

NJIA 7 ZA UHAKIKA ZA KUPATA AJIRA HIZI HAPA


Kupata nafasi za ajira imekuwa ngumu siku hadi siku, hususani ukitilia maanani kuwa wahitimu wanazidi kuwa wengi na hali ngumu ya uchumi inafanya waajiri kushindwa kuongeza nafasi mpya za kazi. Hakuna haja ya kukata tamaa ya kupata kazi ile unayoitarajia hata kama kuna ukiritimba mwingi katika soko la ajira kama vile watu kupeana kazi kwa kujuana, nafasi za kazi kutotangazwa  au kazi haipatikani mpaka rushwa itembee. Makala hii inaenda kujadili mambo ya msingi kwa yeyote anayetafuta kazi, uwe kwa sasa umeajiriwa unatafuta kazi mbadala au uwe hauna ajira unatafuta ajira, bila shaka mambo yanayojadiliwa hapa yatakusaidia.AJIRA

1. Mtazamo wako kuhusu ajira

Fahamu kuwa bidhaa ni chochote kile ambacho kinatimiza mahitaji fulani. Mwenye kuhitaji bidhaa huwa anaitwa mteja.  Muajiri anatafuta mfanyakazi kwa kuwa analo hitaji la kazi fulani kukamilika, na anayo matarajio kadhaa kutoka kwa mfanyakazi anayemuajiri.   Hivyo wewe kama mfanyakazi mtarajiwa unayo ‘bidhaa’, yaani uwezo wako wa kutimiza majukumu fulani ambayo utatakiwa kufanya na muajiri. Kwa hiyo mtazamo sahihi unaotakiwa kuwa nao wakati unatafuta kazi ni kuwa wewe ni muuzaji wa bidhaa, na muajiri wako mtarajiwa ni mteja.  Kwa kuwa wapo ‘wafanyabiashara’ wengi wa hiyo bidhaa kama yako (watu wanaotafuta ajira), unahitajika basi kujipanga vyema ili kumshawishi na kumfanya mteja wako  (muajiri mtarajiwa) aone kweli sababu ya kununua ‘bidhaa’ kutoka kwako.AJIRA

2. Wasifu wako ujitosheleze

Ukiwa na mtazamo ulioelezwa hapo juu wa kuwa wewe ni mfanyabiashara unauza bidhaa kwa mteja wako (muajiri), unatakiwa basi utumie vyema wasifu wako (CV) kujieleza vyema ili ‘mteja’ akukubali. Mambo ya kuzingatia katika wasifu wako ni kama yafuatavyo:-

Wasifu wako uendane na aina ya kazi unayoomba; hivyo basi usiweke kila aina ya maelezo hata yale ambayo haya umuhimu na kazi husika. Mfano unaomba nafasi ya kazi ya uhasibu, lakini unaweka maelezo ya uzoefu wa sehemu tatu tofauti ya kazi za ulinzi.

Wasifu wako uoneshe kweli unao uwezo wa kazi unayoiomba; hivyo basi usitaje tu majina ya kampuni au asasi ulizofanya kazi na aina ya cheo ulichoshika ukiwa huko, bali eleza mambo ya msingi ambayo ni mafanikio ya wewe kuwepo katika kampuni au asasi fulani uliyokuwepo. Mfano kwa kazi yako kama msimamizi wa ofisi, uliweza kuandaa mikutano (itaje) ambayo ilikutanisha watendaji wakubwa wa kampuni yako ambapo kupitia maandalizi mazuri uliyoyafanya, kampuni yako iliweza kupendekezwa mara tatu mfulululizo kuandaa mikutano hiyo.cv

Wasifu wako uoneshe utofauti wako wewe na watu wengine; haitoshi kuandika katika CV yako kuwa umemaliza masomo ya ngazi ya stashahada au shahada, haitoshi kutaja kuwa umewahi kufanya kazi fulani mfano kazi ya usimamizi wa ofisi halafu ukaorodhesha majukumu ya msimamizi wa ofisi, mambo ambayo kwa ujumla yanajulikana kuwa ni majukumu ya msimamizi wa ofisi yeyote yule wa ofisi.

Kumbuka wasifu wako (CV) ni nyaraka muhimu ya kumshawishi ‘mteja’ kuwa ananunua ‘bidhaa bora’ zaidi ya nyingine katika soko la ajira. Hivyo basi jipange kwa kuonesha utofauti, badala ya kutaja tu ngazi za juu za elimu ulizofanikiwa kufika, taja pia maeneo ambayo wewe kweli ‘upo vizuri’ yaani maeneo ambayo kweli haubabaishi katika ngazi hizo za elimu unazotaja. Pia kwa upande wa uzoefu wa kazi, taja mafanikio uliyokwisha kupata kutoka ajira zako zilizopita, au tuseme mambo gani ‘mazito’ ulikamilisha na kusaidia ukiwa kwa waajiri wengine.

3. Fuata maelekezo kwa ufasaha

Unapowasilisha maombi yako ya ajira, hakikisha unafuata maelekezo yaliyotolewa katika tangazo la nafasi za kazi, kwani hata kama ni jambo dogo, utakalokosea linaweza kuchukuliwa kama sababu ya wewe kutokuwa mfanyakazi makini, hivyo kukosa hata nafasi ya kuitwa kwa usahili (interview).AJIRA

Mfano kama umeambiwa uorodheshe wadhamini watatu, hauna sababu ya kuorodhesha wadhamini wawili tu. Kama umeambiwa utume maombi kwa njia ya posta, usitume maombi yako kwa barua pepe wala kupeleka kwa mkono. Hakikisha pia unafuata maelekezo ya tarehe na muda wa kuwasilisha maombi yako ya kazi. Pia zingatia maelekezo kuhusu vyeti na nyaraka nyingine unazotakiwa kuziambatanisha pamoja na barua yako ya maombi ya kazi. Kama umeambiwa utume CV yako tu, usihangaike kutuma vitu vingine kama vyeti na barua ya maombi ya kazi.

SOURCE: MTEMBEZI

ITAENDELEA …

Share:

0 comments:

Post a Comment

Ads

Blog Archive