Friday 25 August 2017

SIMBA YAANZA YANGA YASUBILI

 
Utamu wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL), msimu wa 2017/18 utaanza rasmi kesho Jumamosi Agosti 26, 2017 kwa michezo saba itayochezwa katika viwanja tofauti nchini.
Mabingwa wa Ngao ya Jamii, Simba watashuka kwenye Uwanja wa Uhuru kuwakaribisha Ruvu Shooting kesho Jumamosi, wakati mabingwa watetezi Yanga kesho kutwa Jumapili itakuwa kwenye uwanja huo kukaribisha Lipuli iliyorejea Ligi Kuu baada ya kusubili kwa miaka zaidi ya kumi.
Simba itaingia katika mchezo huo ikiwa na kikosi chake chenye thamani ya Sh 1bilioni wakiwa na lengo moja tu kuthibisha ubora wao na kuonyesha mashabiki na wapenzi wao kuwa msimu huu wataupata ubingwa.
Safu ya ushambuliaji wa Simba chini ya Mganda Emmanuel Okwi bado haijafanya kila kilichotegemewa na wengi hivyo watawajibika kuhakikisha wanafunga mabao mengi dhidi ya Ruvu Shooting na kutuma salamu kwa timu nyingine.
Mabingwa wa Kombe la Mapinduzi, Azam wenyewe watakuwa kwenye Uwanja wa Nangwanda Sijaona mjini Mtwara kuwavaa wenyeji Ndanda FC iliyokuwa na maandalizi duni pamoja na kufanya usajili wa mafungu.
Azam inayoundwa na vijana wengi pamoja na sura mpya itacheza mechi yake ya kwanza ikiwa bila ya mshambuliaji wake John Bocco, kipa Aishi Manula na beki Shomari Kapombe waliotimikia Simba, pia wakiwa na kumbukumbu mbaya kila wanapocheza na Ndanda hivyo wanawajibu wa kuondoa jinamizi hilo.
Singida United iliyopanda daraja kwa mara ya kwanza, lakini usajili wake na uwekezaji mkubwa waliofanya unaifanya mechi yao ya kwanza dhidi ya Mwadui FC kuwa na utamu wa pekee kwenye Uwanja Mwadui Complex, Shinyanga.
Mabingwa mara mbili wa Ligi Kuu, Mtibwa Sugar watakuwa nyumbani kwenye Uwanja wa Manungu, Turiani kuwavaa Stand United wakati Mbao watakuwa wageni wa Kagera Sugar kwenye Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba.
Majimaji itakayosafiri kuifuata Mbeya City kwenye Uwanja wa ya Sokoine jijini Mbeya, huku wageni wengine wa ligi hiyo Njombe Mji ikiialika Tanzania Prisons ya Mbeya kwenye Uwanja wa Sabasaba huko Makambako.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Ads

Blog Archive