Wednesday 19 July 2017

SIMBA YAITOLEA UVIVU YANGA


Beki wa kati wa Simba, Mganda, Juuko Murshid.
MPANGO wa Yanga kukamilisha usajili wa beki wa kati wa Simba, Mganda, Juuko Murshid, hatimaye umeyeyuka baada ya mabosi wa Msimbazi kumuwekea ngumu.
Hiyo ni siku chache tangu ziwepo tetesi za Yanga kumfuata beki huyo nchini Uganda kwa ajili ya kufanya naye mazungumzo ili wamsajili msimu ujao wa Ligi Kuu Bara.
Yanga hivi sasa ipo katika mipango ya kuiimarisha safu yake ya ulinzi baada ya beki Mtogo, Vincent Bossou kuondoka kutokana na kushindwana maslahi.

Kwa mujibu wa taarifa ambazo imezipata Championi Jumatano kutoka ndani ya uongozi wa Simba, beki huyo bado ana mkataba wa mwaka mmoja kwa ajili ya kuichezea Msimbazi.

Mtoa taarifa huyo alisema, Simba haina mpango na beki huyo kutokana na yeye mwenyewe kugoma kurejea kujiunga na timu hiyo huku ukipanga kumuuza sehemu yoyote lakini siyo Yanga.

Aliongeza kuwa, Simba na Yanga hazina ujamaa wa kuachiana wachezaji kutokana na utani wa jadi uliopo kwenye klabu hizo kongwe na pinzani.

“Juuko bado ana mkataba wa mwaka mmoja na Simba, licha ya kutokuwa na mpango naye, lakini hatutakubali kumuachia aende kuichezea Yanga msimu ujao.

“Na ikumbukwe kuwa Simba na Yanga hazina ujamaa wa kupeana wachezaji kirahisi, tena akiwa bado ana mkataba, niseme tumeweka makubaliano kuwa kama mchezaji anataka kuondoka Simba, basi aende kwingine lakini siyo Yanga, labda mkataba wake uwe umemalizika.

“Hivyo, kama Yanga wanamtaka Juuko wasubirie hadi msimu ujao akiwa mchezaji huru lakini msimu huu kujiunga na timu hiyo haitawezekana,” alisema mtoa taarifa huyo.

Alipotafutwa Kaimu Makamu wa Rais wa Simba, Idd Kajuna kuzungumzia hilo simu yake ya mkononi iliita na baadaye kukatwa, gazeti hili halikuishia hapo liliendelea kumtafuta Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya timu hiyo, Said Tully, simu yake iliita na yeye akakata.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Ads

Blog Archive